itunes pic

Karibu wiki moja iliyopita Mhe. Zitto Kabwe alizungumza na jumuiya ya Watanzania waishio Jimbo la Michigan nchini Marekani. Mazungumzo hayo yaliyofanyika wakati wa hafla ya chakula cha jioni aliyoandaliwa Bw. Zitto yaligusia mambo mbalimbali na hasa kuwataarifu wanajumuiya hiyo mambo mbalimbali yanayoendelea nyumbani na pia kusikiliza maoni na maswali yao.

Matangazo ya leo basi ni hotuba ya Mhe. Zitto kwa jumuiya hiyo na sehemu ya maswali na majibu, yote ni uncut and an edited. Makosa mengine yoyote ya kurekodi hasa mwanzoni kidogo ni ya KLHN.

Pichani Mhe. ZItto akijiandaa kuzungumza na wanajumuiya ya TAMI - Tanzanians Association of Michigan. Huko Detroit eneo la Maili Nane.

[PLAY]
itunes pic

Gavana wa Benki Kuu, Dk Beno Ndullu (katikati) akisikiliza maelezo kutoka kwa Meneja wa Benki ya Maendeleo Afrika Mashariki (EADB), Andulile Mwakalyelye (kulia) alipotembelea mabanda wakati wa mkutano wa Makandarasi na Taasisi za fedha kwenye viwanja vya Karimjee Dar es Salaam. Kushoto ni Msajili wa Bodi ya Makandarasi, Mhandisi Boniface Muhegi

Kuna mahali katika serikali yetu watu hawawasiliani. Nina kila sababu ya kuamini kuwa kuna mtu ambaye hafikishi habari kwa mwingine kiasi kwamba tumefikia mahali watumishi wa wizara ile ile na ambao kimsingi wanatakiwa kuwasiliana inaonekana hawawasiliani.

Hebu fikiria, Katibu Mkuu wa Hazina anasimama na kutetea maamuzi yake kuwa alipotia sahihi kwenye kampuni ya Tangold kama mmoja wa wakurugenzi alijua kuwa kampuni hiyo ni mali ya serikali. Siyo hivyo tu aliyekuwa Waziri wa Fedha Bi. Zakhia Meghji aliliambia Bunge kuwa kampuni hiyo iliyochukua nafasi ya kampuni nyingine ya "serikali" ya Meremeta ni mali ya serikali.

Kabla hilo halijatulia Gavana wa Benki Kuu ambayo kampuni hiyo ilimegewa karibu Bilioni 155 kwa vile ni kampuni ya serikali anaibuka kesho yake na kusema kuwa watu wasiihusishe Benki hiyo Kuu na Kampuni hiyo kwani hakuna ushahidi wowote kuwa kampuni hiyo inamilikiwa na serikali

Sasa nani anaweza kuwa na uwezo wa kujua juu ya Kampuni hii kati ya Katibu Mkuu Hazina ambaye ni Mkurugenzi wa Tangold na Gavana wa Benki Kuu iliyotoa mabilioni kwa taasisi hiyo?

Hivi Watanzania tumekosa nini hadi tuburuzwe kama watoto wanaochezewa mchezo wa Karata tatu? Hivi mtu akimuuliza Kikwete kama Kampuni ya Tangold ni ya serikali atakuwa na jibu kweli wakati Hazina na Benki Kuu hawakubaliani?

Hili nalo linanikumbusha juu ya Mgodi wa Buhemba ambao tuliambiwa kuwa ni mali ya serikali lakini Mkaguzi Mkuu wa serikali anasema hana jina hilo katika orodha ya makampuni ya serikali. Sasa mgodi huo unalindwa na Polisi, nani anaumiliki?

Kuna mtu yeyote anaweza kutoa jibu? Hivi kweli tumefikia mahali hatujui hata nani anamiliki mgodi mkubwa kama Buhemba? Hivi tukiuliza nani anamiliki Ikulu yetu tunaweza kuwa tunatafuta ugomvi? Tukisema kuna mafisadi hivi kweli watakuwa na sababu ya kututafuta? Au tuanze kampeni kwa kupitia wahisani dhidi ya misaada au tutaambiwa tunataka watu wa kawaida wapate shida? Ni nini kitatufanya tuchore mstari?

Naomba nitoe wito kwa Waziri wetu wa Fedha atuambie bila kujiuma uma, ni nani anamiliki Tangold na Buhemba? is this too much to ask as citizens of our beloved country au ndio imekuwa ni mradi wa Usalama wa Taifa?

itunes pic

Mbunge wa Igunga Mhe. Rostam Aziz (CCM) ameamua kulishtaki gazeti la Mwanahalisi na wakati huo huo kulitishia gazeti la Raia Mwema kuwa atalifungulia mashtaka endapo halitaomba radhi kwa mojawapo ya makala zake.

Bw. Rostam anakuwa kiongozi wa kwanza ambaye amekuwa akitajwa na vyombo vya habari kuhusu ufisadi aliyeamua kwenda mahakamani. Kwa namna ya pekee hli linaashiria mambo kadhaa.

Kwanza, endapo mahakama itaridhia maombi yake basi masuala ya Richmond na Rostam yanaweza yasitajwe kwenye sentensi moja kwani kesi itakuwa mahakamani . Huu ni mchakato wa Kisheria na vyombo husika vitatakiwa kuheshimu, ingawa hilo halitufungi sisi wengine kutolea maoni

Pili, kujaribu kunyamazisha vyombo hivyo vya habari endapo kutakubaliwa na mahakama basi kutazuia habari mpya kuweza kuchapwa na gazeti hilo . Hata hivyo, sisi wengine tutaweza kuendelea kutolea maoni

Jambo la tatu ni kuwa Bw. Rostam amefanya jambo la maana kwa kuamua kwenda mahakamani hasa kwa vile anaamini haki yake inatishiwa na jina lake kuchafuliwa. Hivyo, uamuzi wake ni mfano wa kuigwa kwa wengine ambao wanahisi kuonewa au kutotendewa haki ili watumie vyombo vya sheria kutafuta haki hiyo badala ya kukimbilia kwenye TV au radio kujisafisha.

Hata hivyo, kama kesi hii itanedelea au itaishia pembeni hatuna uhakika. Hata hivyo vyanzo vyangu vya karibu na MwanaHalisi vimenihakikishia kuwa hawana mpango wa ku "back down" na wanaendelea kufanyia kazi taarifa nyngine kuhusu Rostam na Richmond. Sisi wengine yetu ni macho tu.

Je wadaiwa wengine na wale wanaotajwa kwenye tuhuma za ufisadi na wenyewe waende mahakamani? Je ndiyo njia pekee ya wao kujisafisha? Kwanini wale wengine waliotishia kwenda mahakamani hawakwenda?

itunes pic Kwa karibu wiki mbili sasa nimekuwa nikitengeneza hoja na kumulika kama vile kurunzi idara ya Usalama wa Taifa. Sikiliza introduction ya makala yangu maalum kwenye gazeti la "Kulikoni" leo. Kwa wale ambao hampo nyumbani makala hii itawekwa baadaye mchana wa Ijumaa (saa za Marekani) kwenye http://www.klhnews.com upande wa editorial.
[PLAY]
itunes pic

Ndugu zangu, kuna uwezekano mkubwa kwamba itakapofika kiangazi mwaka huu, Taifa letu linaweza kujikuta kwenye upungufu mkubwa wa chakula ambao siyo tu unatishia maisha ya watu wetu bali pia unashusha hadhi na utu wa mwanadamu. Hakuna kitu kinachomdhalilisha mwanadamu na kuweza kumfanya awe mtu kama njaa.

Ni njaa ndiyo inayoweza kumfanya mtu aukane urithi wake wa kwanza kama alivyofanya Esau na ni njaa ambayo ilikuwa inatumika tangu enzi za kale kama silaha ya mwisho ya vita ambayo inalazimisha watu kusalimu amri.

Tanzania tutakabiliwa na njaa ambayo chanzo chake si ukame. Mara nyingi (kama siyo zote) njaa husababishwa na ukame na vita. Hata hivyo njaa ambayo naweza kuiangalia toka mbali na inayosogelea kama simba anyatiaye haitokani na mambo hayo bali makubwa mawili.

a. Kupanda kwa bei ya chakula duniani.
Habari za leo ni kuwa bei ya chakula duniani imepanda kwa haraka kuliko wakati wowote ule na hivyo kusababisha ugumu wa kupatikana kwa chakula. Yaliyotokea Haiti na Misri siku chache zilizopita ni dalili ya ubaya wa hali hiyo. Kwa wale walioko Dar au maeneo yenye masoko ya kudumu na kwenye mialo mbalimbali kanda ya ziwa wanaweza kutusaidia kutuambia kama kumeanza kutokea mabadiliko yanayoonekana ya bei ya chakula siku hizi chache zilizopita.

b. Mvua ya masika.
Hata hivyo naamini kwa upande wa Tanzania kitakachosababisha njaa sana ni hii mvua ambayo imeharibu mashamba na mazao ya watu kiasi kwamba baadhi ya maeneo ambayo kwa kawaida yana chakula cha kutosha yanaweza kujikuta yanahamia mwaka huu. Kama mpunga wa Kyela utakuwa umeathirika kama Dr. Mwakyembe alivyosema kwenye mahojiano yake nami kuna uwezekano kuwa Mwaka huu bei ya Mchele nayo itapanda na hivyo kufanya nafaka hiyo ianze kuwa adimu na kupatikana kwa wachache.

Maeneo ambayo mchele ndiyo chakula kikuu na pia zao la biashara watajikuta wanakabiliwa na upungufu wa fedha za kununulia hata vitu vingine na hivyo kusubiri chakula cha misaada.

Kwa vile tunajua haya yote na ziada; tufanye nini ili tujiandae na njaa ijayo?

itunes pic

Hadi gazeti la Guardian litutangazie kuwa Waziri wetu ameficha Bilioni kisiwani Jersey (thanks Yebox2) wao kina RO walikuwa wapi?

Hadi Kamati Teule ilipotuambia rasmi kuwa RDC ni kampuni hewa RO na timu yake walikuwa wapi?

Niendelee kuorodhesha ushahidi wa uzembe uliokithiri na uvivu wa kufikiri wa taasisi nyeti ya Usalama wa Taifa? Kama wameshindwa kugundua matukio ya economic sabotage yanayoendelea nchini wana faida gani? Hii ya kusafiri na Rais na kutumia vi ear pieces na makoti marefu kama vile wao Secret Service?

Kwanini basi Mkurugenzi wa Idara hiyo Bw. Rashid Othman (Pichani) asijiuzulu kwa ajili ya Usalama wa Taifa!!!

Lakini kabla yake Bw. Cornel Apson Mwang'onda na yeye alishikiri vipi katika kuzembea kulilinda Taifa letu na ni nani mwenye ujasiri wa kumuita na kumhoji?

Isije kuwa Usalama wa haki ya kula na kutanua na fedha za walipa kodi wa Tanzania lakini inapokuja katika kuelezea walifanya nini na pesa hizo inakuwa mbinde?

yes I said it!

itunes pic

Ni kweli yawezekana kuwa kujiuzulu Uwaziri kumepokelewa kwa furaha na wengi (mimi mmoja wao). Yawezekana kwa kufanya hivyo uchunguzi utakuwa huru (sidhani alikuwa anazuia uchunguzi anyway); yawezekana kujiuzulu kwake kumekuwa ni kitulizo cha kelele dhidi ya ufisadi; Yawezekana kujiuzulu kwake kumeonesha ufisadi wa viongozi wa serikali ya JK na hivyo kumuondoa kumeonesha jitihada za kusafisha serikali hiyo;

Hata hivyo, hadi hivi sasa CCM haijalipa gharama yoyote ya viongozi wake kuhusishwa na ufisadi na hakuna wakati hadi hivi sasa ambao wao kama CCM wamechukua hatua za viongozi wa serikali waliofanya vitendo vya ufisadi wakiwa ni wanachama wake.

Ni kwa sababu hiyo basi naamini kujiuzulu kwa Chenge toka serikalini hakutoshi bali lazima kufuatiwe na kujiuzulu toka Ubunge. Kwanini?

a. Kiasi cha fedha anachodaiwa kukutwa nacho kingeweza kuleta mabadiliko makubwa kwa watu wa Jimbo lake lakini aliwaficha wapiga kura wake.
b. Kwa kukiita kiasi hicho "vijisenti" kwa kisingizio cha "usukuma wake" ni tusi kwa wasukuma wengine ambao hawajui maana ya "vijisenti" hasa baada ya yeye mwenyewe kuelezea kuwa "kila mtu ana kiwango chake".
c. Mwakilishi wa wananchi anapotajwa na kuhusishwa na kitendo cha matumizi mabaya ya nafasi yake, nafasi ambayo imetokana na kuchaguliwa na wananchi hao, basi anapojiuzulu nafasi yake basi hana budi kuachia kiti chake ili ampishe mtu mwingine kushika nafasi hiyo.

Bw. Chenge amewaangusha wapiga kura wake, na amekiletea aibu kubwa chama chake. Kati ya wote walioatajwa katika tuhuma za ufisadi ni yeye pekee ambaye tunajua angalau kiasi gani che fedha kimefichwa huko Jersey. Kwa sababu hiyo basi Chenge siyo tu ajiuzulu Uwaziri kama alivyofanya bali pia ajiuzulu Ubunge wake na Uwakilishi wake ili mwana CCM au mtu mwingine aweze kuwawakilisha wananchi wa Bariadi Magharibi.

JIUZULU UBUNGE BW. CHENGE, UMEKUWA AIBU YA TAIFA LETU!

PIcha na Mpoki

itunes pic Chenge ni bilionea wa kutupwa ambaye kwake shilingi Bilioni moja anayodaiwa kuificha huko Marekani ni sawa na "vijisenti" vichache. Hivi tatizo letu liko wapi? Je yawezekena kuwa chenge ni dalili tu ya tatizo? Je eye ni kiongozi pekee wa TAnzania ambaye amewekeza mabilioni ya shilingi kwenye akaunti za kigeni? Je ajiuzulu au na yeye anaweza akalia kuwa amefanywa "Bangusilo" wa rada!?
[PLAY]
itunes pic Sakata la Richmond na mtikisiko wake bado havijaisha Bungeni. Kuna kila dalili kuwa yaliyotokea Bungeni mwezi wa pili na kusababisha kujiuzulu kwa Waziri Mkuu na kuvunjika kwa baraza la Mawaziri hayakuwa mwisho. Kuna kila dalili kuwa kuna baadhi ya watu ambao waliumizwa na hadi hivi sasa hawajakubali "yaishe"

Miongoni mwa watu ambao kwa hakika waliumizwa hisia zao, hadhi na sifa zao ni Mbunge wa Igunga Mhe. Rostam Aziz (CCM) ambaye wakati wa matukio hayo alidai kuwa ripoti iliyosomwa na Mwenyekiti wa Kamati Teule ya Bunge Mhe. Harrison Mwakyembe (Kyela - CCM) haikuwa sahihi na akadai kama vile wengine kuwa hakutendewa haki.

Juhudi za kujisafisha kwa wahusika mbalimbali wa Richmond zimekuwa zikiendelea na kwa namna fulani jukumu kubwa zaidi linamuangukia Bw. Rostam ambaye aidha kwa kujitwisha mwenyewe au kukubali kutumika inaonekana amekuwa akitumia kila aina ya njia upande mmoja kujibu mashambulizi ya wapinzani kwa kutumia vyombo vyake vya habari na upande wa pili kutilia shaka utendaji mzima wa Kamati Teule na hivyo kujaribu kuhoji maamuzi yote yaliyotolewa Bungeni

Katika kikao kinachoendelea cha Bunge alitakiwa aje kutoa maelezo yake na kujibu hoja za Wabunge na kutoa utetezi wake. Mwishoni mwa juma alikuwa amejiandaa kutoa utetezi huo lakini kwa kile kinachodaiwa kuwa ni "unyeti" wa utetezi wake basi imeonekana si vyema kwa Bw. Rostam kujitetea Bungeni kwani italeta msukosuko mwingine nchini

Kama hilo ni kweli au ni mojawapo ya karata za CCM binafsi siamini kuwa Rostam anaweza kusema chochote kile ambacho kinaweza kutuyumbisha kama Taifa na ambacho hatuwezi kukihimili. Tumeweza "kuchafuka kwa hali ya kisiasa Zanzibar", tumeweza kuhimila msiba wa Sokoine, tumeweza kuhimili "mizengwe" ya Kizota na kifo cha Katibu Mkuu Kolimba na kwa hakika tumeweza kuhimila kujiuzulu kwa WAziri Mkuu

Naamini nchi yetu inaweza kuhimili msuko suko wowote ule wa kisiasa hata kama ni kujiuzulu kwa Rais aliyeko madarakani! Hata ikibidi Bunge zima kujiuzulu au kuvunjwa na kuitisha uchaguzi mwingine, TAifa letu lina uwezo wa kuhimili mambo hayo kwani Taifa ni kubwa zaidi kuliko kikundi fulani cha wanasiasa.

Wito wangu leo ni kuwa kama Rostam analo la kusema na aliseme sasa asinyamazishwe tena wala kupigwa mkwara na chama chake. Kamas anaona hakutendewa haki yeye kama Raia basi anayo haki ya kujisafisha hadharani badala ya kulazimika kukaa kimya. Asije akafikiri kuwa ana mpango wa kuzungumza "huko mbeleni" lakini ikatokea kuwa yeye na utetezi wake wakanyamaza "milele" kama alivyonyamaza Bi. Amina Chifupa ambaye naye alitaka kupewa nafasi ya kujitetea lakini akazibwa mdomo. Natoa wito; kama Rostam unaamini una hoja SIMAMA JITETEE NA JIELEZE

Lakini swali kubwa ni Rostam ana nini ambacho kinampa nguvu ya kutia mwashawasha Bungeni? Je anatikisha kiberiti kuona kama kimejaa

itunes pic

Pichani baadhi ya wananchi wakijaribu kuvuka mto. Kidaraja hicho sasa hakipitiki tena. Picha kwa hisani ya Mjengwa

Mvua za masika zimezidi kupamba moto nchini na zimekuwa zikisababisha mafuriko sehemu mbalimbali. Baadhi ya maeneo ambayo yamepata mafuriko ni pamoja na Vunjo, Same na Kyela. Hata hivyo hadi hivi sasa ni wilaya ya Kyela ambayo ina kata 15 ambazo kati ya hizo 11 zimepatwa na mafuriko makubwa .

Siku ya Jumamosi nimepata nafasi ya kuzungumza na Mbunge wa Jimbo la Kyela Dr. Harrison Mwakyembe (CCM) kuhusu athari za mafuriko hayo na mahitaji ya msaada. Kwa kifupi hali ilivyo ni kuwa:

a. Kaya 9000 hazina mahali pa kuishi, zimekosa chakula, au athari ya moja kwa moja iliyotokana na mafukio hayo

b. Hadi hivi sasa watu wawili wamefariki

c. Madhara makubwa katika mashamba ya mpunga kiasi kwamba kuna uwezekano kuwa kwa mara ya kwanza Kyela itahemea chakula mwaka huu.

d. Mvua kubwa namna hii hazijawahi kunyesha Kyela kwa karibu miaka thelathini sasa.

e. Juhudi za kuleta misaada zinaendelea ambapo JWTZ imepeleka kikosi chake cha Uhandisi, huku Msalaba Mwekundu wakiandaa misaada ya vitu mbalimbali.

Dr. Mwakyembe anaomba msaada wa Watanzania wote popote pale walipo kuweza kusaidia wananchi wenzao ambao ni kama wamepatwa na "Kimbunga cha Katrina" kwani wengi sasa wanaishi makanisani na kwenye mashule na afya zao ziko hatarini hasa kutokana na uwezekano mkubwa wa kuibuka mlipuko wa magonjwa yanayoambukizwa kwa maji kama typhoid, kuhara damu, salmonella, na pia ongezeko la Mbu wasababishao Malaria.

Kwa yeyote aliyeko Dar, unaweza kutuma mchango wako kupitia:

Kyela Development Fund MNB Bank House Acct No: 2013300198

Au Wasiliana na Dr. Mwakyembe kupitia simu Namba: 255 754 284130

kwa maelekeo ya kuweza kutoa mchango wako kupitia yeye mwenyewe

Tafadhali sikiliza mahojiano yangu na Dr. Mwakyembe. KLH News imeahidi kutoa msaada wa Shilingi laki mbili kama sehemu ya jitihada za kuwasaidia wananchi wa Kyela

[PLAY]