June 29, 2009 07:17 PM PDT
Kwamba Rais mstaafu Mkapa alitumia madaraka yake vibaya alipojipatia yeye na aliyekuwa Waziri wa Nishati na Madini Daniel Yona Mgodi wa Kiwira halina shaka. Kwamba katika kufanya hivyo alivunja Katiba na alipaswa kuondolewa madarakani kwa mujibu wa ibara ya 46 ya Katiba kwa kuvunja vipengele kadhaa vya sheria ya maadili ya viongozi wa umma ya 1995 na mabadiliko yake nalo halina shaka.
Chenye kuleta tatizo ni jaribio la serikali ya sasa kufanya makosa aliyoyafanya Mkapa akiwa madarakni kuwa ni kama "bahati mbaya" au "kupitiwa". Tatizo wanalolileta ni kuwa sheria haipaswi kufuatwa na watu wote na mtu ambaye ni Rais basi anaweza kufanya lolote atakalo akijua kuwa atatetewa.
Uamuzi wa kurudisha Kiwira mikononi mwa serikali ni ushahidi wa wazi kuwa Mkapa alifanya makosa ambayo kimsingi ukiunganisha na mambo mengine yalikuwa ni ya uvunjaji wa sheria na kwa hakika yangempasa afikishwe mahakamani kujibu mashtaka mazito dhidi yake.
Hata hivyo, Waziri Mkuu Pinda anasema mataifa ya nje yanamtambua na kumpenda Mkapa kwa kuwa ni mtu mwadilifu. Na zaidi ameliambia taifa kuwa anaamini kuwa Mkapa si "fisadi" kwa vile hana akaunti za dola nje ya nchi wala mandege yanayorushwa nchini.
Hivi ni nani alimuambia Mheshimiwa Pinda kuwa tatizo la ufisadi nchini ni watu kuwa na akaunti nje ya nchi? Kama hilo ni kweli anasema nini kuhusu Chenge ambaye ana akaunti ya mamilioni huko Uingereza na bado ni Mbunge?
Nimeandika kwa kirefu juu ya hili na ninatumaini itakuwa kwenye mojawapo ya magazeti ninayoandika siku ya Jumatano. Maswali ambayo natafuta majibu yake:
Ni kitu gani kitakufanya uridhike na kumsamehe Mkapa kwa kitendo chake? Je kurudisha Kiwira serikalini inatosha (kama vile aliyeiba ng'ombe akirudisha asishtakiwe kama wale wanaodaiwa kurudisha fedha za EPA?)
Je, sheria ifuate mkondo wake hata kama mhusika ni Rais mstaafu au tusiwaguse viongozi wetu wastaafu hata kama tunajua wamevunja sheria? Itakuwaje kama huko mbeleni tuje kusikie baadaye kuwa Rais fulani alipokuwa madarakani alimbaka mtumishi wake wa ndani, je tutamuachia kwa vile ni mstaafu?
NB: Ninafanya mambo kwa kibaba kutokana na hali ngumu ya uchumi kama mjuavyo japo kuna mambo mengi sana ya kufanya na kwa wale wanaojua mipango yetu KLHN kwa kweli sasa hivi tuko nyuma kwa karibu miezi mitatu. Tunaomba dua na sala zenu ili tuweze kufanikisha mipango yetu ili kuelekea 2010 mwamko mpya wa fikra uzidi kujikita miongoni mwa watu wetu.
June 10, 2009 10:40 AM PDT
Ifuatayo ni taarifa ya habari ya saa mbili za Usiku Juni 10, 2009 kwenye TBC
June 08, 2009 10:15 PM PDT
Kwa usiku kucha kundi la wahuni waliojibatiza jina la "wanakijiji" na kutuchafua wengine walivamia eneo la Mhe. Aloyce Kimaro (Vunjo-CCM) na kuharibu mazao na kuchoma nyumba na kuiba mali mbalimbali, walifanya hivyo kwa kile ambacho gazeti la Mwananchi limeelezea kuwa "wanadai kwamba, kwa kuwa shamba hilo liko katika eneo lao wangepewa ili walitumie kwa shughuli mbalimbali ikiwemo kujenga shule, hivyo kitendo cha serikali kuliuza kwa mtu wa nje ya kijiji hicho ni kunyanganya haki yao."
Kitendo hiki ni cha aibu na kina fanana na vitendo vya uvamizi kule Zimbabwe au vile vilivyosababisha machafuko makubwa Kenya vya Mungiki. Ni vya kulaaniwa na kila mpenda haki na mwenye kuheshimu utawala wa Sheria.
Ni kwa sababu hiyo tumepata nafasi ya kuzungumza na Bw. Kimaro jana kuhusu suala hili na kujaribu kutafuta maoni yake na kama kitendo hiki kitamfanya ahamishe uwekezaji huo wa Arumeru na kuupeleka sehemu nyingine kwani hawamtaki huko Arumeru!
Sikiliza:
June 07, 2009 09:43 PM PDT
Siku ya Jumamosi nilialikwa kuwa mmoja wa wachangiaji katika kipindi cha "Tulonge Asubuhi" kinachorushwa na Star TV Jijini Mwanza. Mada kuu ilikuwa tulilojifunza kutokana na Uchaguzi mdogo wa Busanda.
Wachangiaji wengine ambao nao walipata nafasi ya kuchangia kwenye onesho hilo la asubuhi ni pamoja na Erasto Tumbo (Chadema), na Amos Makalla (CCM) pamoja na wapiga simu wengine.
Ni matumaini nitaendelea kupata nafasi kama hii ili kuendelea kuchochea mabadiliko ya kifikra ambayo mara zote hutangulia mabadiliko ya kura!
Unaweza kuniandikia: mwanakijiji@mwanakijiji.com
May 17, 2009 11:02 PM PDT
Unaweza kusikiliza kwa kudownload kutoka hapa au kusikiliza moja kwa moja kwa kubonyeza "play" chini hapa.
http://www.box.net/shared/qfp38sfr3n
Ukisikiliza usiniulize, na wala usimwambie mtu mwingine. For your Ears Alone!
M.M.
May 07, 2009 09:25 PM PDT
Ningeweza kukuambia kilichomo lakini sitakutendea haki; itabidi usikilize mwenyewe.
May 06, 2009 09:42 PM PDT
Ni mgongano wa kihistoria ambao ulipaswa kutokea. Ni mgongano ambao hutokea mahali popote panapokuwa na tofauti kubwa kati ya watawala na watawaliwa. Ndivyo ilivyokuwa kwenye Mapinduzi ya Ufaransa, Mapinduzi ya Marekani na Mapinduzi ya Bolshevik (Urusi).
Ni yale yale yaliyotokea na kusababisha mapinduzi ya Cuba yaliyomuingiza Castro madarakani. Ndiyo! Ni yale yale yaliyotokea pia kwenye mapinduzi ya Zanzibar!
Migongano ya namna hiyo asili yake mara zote ni pale wananchi wanapotambua kuwa hawana usawa na watawala wao na ya kuwa tofauti ya maisha yao na yale ya watawala ni kubwa mno na ya kwamba mwananchi wa kawaida anajikuta hana nafasi yoyote aidha ya kufanikiwa au ya kuweza kuishi maisha yenye utu, usawa, haki na heshima.
Nchi chache zimeweza kupitia mgongano huo kwa njia ya nguvu (kama mifano niliyotoa) au kama ilivyotokea huko Ukraine na Georgia miaka ya karibuni kwa njia ya nguvu ya umma.
Tanzania yetu inapitia mgongano huo katika hatua zake za awali. Silaha ambayo wananchi wanatumia leo hii ni nguvu yao ya hoja na wanatarajiwa kubadilisha serikali yao kwa nguvu ya kura.
Hata hivyo hilo halitakuwa rahisi kwani dalili yote inaonesha kuwa watawala hawako laini kuruhusu mabadiliko makubwa ya kiutawala yenye kupendelea wananchi wa kawaida. Hivyo, mgongano unaendelea. Swali ni nani ashinde? Na ni nani ataamua mshindi!?
Nisikilize:
April 29, 2009 11:32 PM PDT
Kwa namna fulani tunaamini kuwa sisi tuna upendeleo wa aina fulani kwa Mwenyezi Mungu, kwamba nchi yetu kwa sababu upendeleo wa pekee basi haitapata majanga. Hatujajifunza kwa ajali zinazotea mara kwa mara za mabasi, hatujajifunza kwenye ajali za majini, hatujajifunza kwenye milipuko ya mabomu na kwa hakika tuko kama tumepigwa ganzi ya aina fulani hivi.
Pamoja na kutoa pole na rambirambi, ni lazima tujiulize tutaendelea mpaka kulini kwa kutegemea rehema za Mungu? Sitoshangaa leo tutaambiwa katika Hotuba ya Rais kuwa haya yalikuwa ni mapenzi ya Mungu na ya kuwa wanaunda tume kuchunguza kitu gani kilisababisha na wananchi wasiwe na wasiwasi hali ni shwari na halikuwa tukio la kighaidi..
Katika wazimu wetu tutasema Amen.. na kusahau kabisa mlolongo wa kutojiandaa na majanga ambao serikali ya CCM imeuendeleza kwa miaka kadhaa sasa na kutuacha tuishi kwa bahati!
Jana, tumeikwepa risasi! Huko mbeleni (na itakuwa hivyo kwani majanga yataendelea kutokea hata kama tunaombea yasitokee, ndiyo kanuni ya ulimwengu!) tutakuja kulia kama tulivyolia kwenye MV. Bukoba na Bahi! (wengine wanajiuliza "Bahi?"! wameshasahau!
April 21, 2009 08:45 PM PDT
Salaam,
Suala la DECI ni marudio tu ya michezo mingine kama hiyo ambayo imeshawahi kutokea huko nyuma. Jinsi suala la DECI lilivyoshughulikiwa linaonesha ni wazi hakuna utaratibu mzuri wa kushughulikia michezo hii na inakuwa kama tunaanza moja. Hatuelewi ni kwanini michezo hii inarudiwa rudiwa hadi inafikia inapofikia ndio kama watu waliokurupushwa watendaji wa serikali ndio wanaanza kufanya kazi.
Twende na tuwe cheche!
April 15, 2009 07:56 AM PDT
Salaam, Pamoja na habari mwanana za wiki hii ambazo zitagusa fikra zako na maoni ya kuthubutu ambayo huwezi kuyapata mahali pengine popote tunakuletea pia habari zinazoendelea kila wakati. Kwa kupata email ya habari mpya na kupokea kijarida chetu cha "Cheche" kwa kutumia barua pepe tuandikie kwenye anuani ya mhariri iliyoko kwenye kijarida.
Kuna habari mbili kubwa ambazo zimeanza kusikika saa hii:
a. Wakuu wa Mikoa wapanguliwa na kubadilishana vituo mbalimbali, hii inaonesha kugusa mikoa ya Tanga, Dar, Iringa, Kilimanjaro, Dodoma n.k Kimsingi siyo habari kubwa inayostahili kwani kilichofanyika ni kubadilishana ofisi tu. Aliyeshindwa eneo moja kumpeleka jingine hakuondoi tatizo ambalo ni yeye! Baadhi ya mabadiliko hayo:
Dr. Ishengoma toka Pwani kwenda Ruvuma
Bi. Hajjat Amina Said toka Iringa kwenda Pwani
Bw. Abdulazziz toka Tanga kwenda Iringa
Bi. Monica Mbega toka Ruvuma kwenda Kilimanjaro (huyu ni yule Mkuu wa Mkoa wa "Kamtumbwi ka Kikwete")
tunaendelea kufuatilia kujua wa Kilimanjaro ameenda wapi na kama Mbeya wamebadilishiwa (maana na siasa zao huko ni vurugu kuwa na Mkuu wa Mkoa ambaye ni mwenyeji wa huko!)
b. Kuna habari kuwa ofisi za DECI zimefungwa au DECI yenyewe imesimamishwa. Utaona katika toleo letu la leo tulitoa wito huo kwani kuiacha kuendelea kufanya kazi katika mazingira ya sasa ni kulea uovu. Kwa hiyo tunasubiri tuone mwitikio utakuwaje kwani tangu makala zetu mbili (iliyotoka kwenye Cheche wiki iliyopita) na iliyotoka leo kwenye Mwanahalisi kuna watu wamechukizwa na wengine wameapa kufanya vitu vibaya endapo DECI itafungwa. Tunatumaini vikosi vyetu vya usalama viko tayari kusimamia haki.
Na hii ni habari ndogo
c. Kwa wakazi wa mikoa ya kanda ya Ziwa, wiki hii wataanza kuona gazeti jipya la habari na maoni na tunarajia kuwa na makala za Mwanakijiji humo pia. Kaeni chonjo.
Basi na sisi na twende na tuwe "Cheche"!
Jipatie nakala ya cheche: http://www.forums.mwanakijiji.com/showthread.php?t=729